Sunday, 15 January 2017

MWINGA KIKOROMEO

Mwinga wetu mamboleo, mwinga semi nyodo nyundwa
Mwinga domo kisemeo, kisa mwanetu kapendwa
Mwinga kinywa kichembeo, wakweze kutwa kusundwa
Mwinga ni kikoromeo, mwinga huyu hakufundwa!
Mwinga huyu shaitwani, mwinga binti ibilisi
Achukiaye jikoni, mwinga mpenda Chipsi
Asoficha maungoni, mwinga zi wazi hipsi
Mwinga ni kikoromeo, mwinga huyu hakufundwa!
Mwinga kutwa fesibuku, mambo tachitachi ati
Mwinga si wa bukubuku, kumi kumi zake noti
Asopenda chukuchuku, mwinga ni kuku rosti
Mwinga ni kikoromeo, mwinga huyu hakufundwa!
Mwinga ni nusu adabu, ni kichomi cha mapafu
Husonya hata mababu, wakwe zake ni wachafu
Mwinga haoni aibu, kufanya yanayokifu
Mwinga ni kikoromeo, mwinga huyu hakufundwa!
Mwinga huyu katushinda, tumechoka vumilia
Vile yeye kampenda, mwanetu twamlilia
Mwinga huyu ni kidonda, dawa kisichosikia
Mwinga ni kikoromeo, mwinga huyu hakufundwa!

No comments:

Post a Comment