Tuesday, 1 September 2015

UJANA


Maisha ni neno pana, Maanae sifukui
Mapacha weza fanana, Kwenye kiza huwajui
Hodihodi waungwana, Nivalisheni kikoi
Ya jana mpe kijana, Uzee asitumai


Ya jana ndo ya ujana, Mzee sijisumbui
Hapo maisha hubana, Na kuhisi hupumui
Shida zikafumukana, Mithili utandubui
Ya jana mpe kijana, Uzee asitumai

Starehe za ujana, Mengi hauyang’amui
Hasa upatapo bwana, Hufanya hujitambui
Ila mtapotengana, Maziwa taona tui
Ya jana mpe kijana, Uzee asitumai

Ujana kubwa hazina, Kama mlima sinai
Ukicheza danadana, Hilo kosa la jinai
Mwisho chochote hakuna, Uzee utakudai
Ya jana mpe kijana, Uzee asitumai

Leo ilikua jana, Wakati hauzubai
Tumia vyema ujana, Dhalili nakupa rai
Ujana ulevi bwana, Uzee ni jitmai
Ya jana mpe kijana, Uzee asitumai

Tamati ninafikia, Mbele tena sisogei
Vyema ujana tumia, Afya isikulaghai
Usije ukajutia, Uzee ukisabai
Ya jana mpe kijana , Uzee asitumai

LIMETUNGWA NA NASRI KIONE
0752300012 nasriibrahimu@gmail.com
(FB) TUNGO ZENYE ULIMBO

No comments:

Post a Comment