Tuesday, 1 September 2015

DENGU

Naona nyote mwang'ara, niwekeni muangani,
Nijitokeze jahara, ya sawa niyabaini,
Sina budi imi jura, kuwauza kilingeni,
Kwa ndimi zenu na sura, dengu ni za rangi gani?


Kwa nyugwe nawazingira, mtamke kwa lisani,
Nyote wa pwani na bara, mlotanganyika ndani,
Nizingapo sina dira, akilini na matoni,
Kwa ndimi zenu na sura, dengu ni za rangi gani?

Msifate ya bendera, pepo zenu zifanani,
Tamkeni bila jera, kwa aswili zenye tani,
Tamka msi izara, tata hini tatueni,
Kwa ndimi zenu na sura, dengu ni za rangi gani?

Zitieni ndimi ghera, mtamke ranji hini,
Nafaka yenye ubora, wa zihi za muilini,
Tena haina madhara, ni ya aswili shambani,
Kwa ndimi zenu na sura, de ngu ni za rangi gani?

Mafaswiha wa busara, zuo zenu angazeni,
Hayano kwenu ibura, mliokwima mbeeni,
Hela msiete tara, ranji hini tujuzeni,
Kwa ndimi zenu na sura, dengu ni za rangi gani?

Yakubu Ngumbao Julius
''moto wa kifuu''
4-8-2015
Nairobi- Kenya

No comments:

Post a Comment