Thursday, 28 May 2015

SINA HAKI YA KUPENDA

SINA HAKI YA KUPENDA

Kwako mola shitakia, Dua zangu pokea,
Binadamu wachekea, umbile langu sikia,
Ufupi lonipatia, kunitusi wanambia,
Jamani mtu mfupi, hana haki ya kupenda?

Ni majuzi litokea, kisa kilonifikia,
Mrembo alinambia, huba kwangu futilia,
 Weye nyundo sikia, kukupenda najutia,
Jamani mtu mfupi, hana haki ya kupenda?

Mie ninazo hisia, kama warefu sikia,
Yarabi hakukosea, ufupi nakunumbia,
Mola unampangia, maumbile kashifia,
Jamani mtu mfupi, hana haki ya kupenda?

Swali ninaulizia, malenga kunijibia,
Moyoni ninaumia, ninashindwa vumilia,
Matamshi lonambia, maulana nakwachia,
Jamani mtu mfupi, hana haki ya kupenda?

Miaka imewadia, ninyi nyundo kubakia,
Twiga wameshaingia, naona mutaumia,
Ninaanza kujutia, ufupi livyonijia,
Jamani mtu mfupi, hana haki ya kupenda?

Sio ninakwingilia, ukanamba nimevia,
Kiapo nakuapia, uliyanena sikia,
Rafiki sitokataa, japo mawi linambia,
Jamani mtu mfupi, hana haki ya kupenda?

Tamati Rama nalia, machozi yabubujia,
Nenda kwetu kutulia, dhiki imenivamia,
Yaillah yajalia, Jalie alo sawia,
Jamani mtu mfupi, hana haki ya kupenda?

RAMADHAN MWARUWA NYAE
“MALENGA MTI MGUMU”
MENZAMWENYE – LUNGALUNGA.

No comments:

Post a Comment